St. Augustine University of Tanzania-Songea

St. Augustine University of Tanzania-Songea
Creating a peaceful society

Thursday, May 21, 2015

Migogoro ya Ardhi sawa na Mgema Tembo kuangushwa na Tawi Alilozoea

Na Wanafunzi  wa Mwaka wa Pili 2015


MIGOGORO ya ardhi Tanzania sawa na mgema tembo anayeangushwa na tawi alilozoea kukalia kila siku wakati wa ugemaji wa pombe hiyo inayotokana na mnazi.

Ebu fuatilia makala hii ili uweze kupata kujuwa ni nongwa gani inayokwamisha kupatikana kwa suluhisho la kudumu kuhusu migogoro ya ardhi chini ya kivuli cha jua la nchi ya Tanzania.

Katika kudhihirisha hilo, afisa Mifugo mkoa wa Ruvuma Dk. Ramadhani Mwaiganju anaeleza kwamba, kwa kawaida inapotokea kufanya kazi kwa mazoea bila kuweka mikakati na njia madhubuti za kudumu kudhibiti migogoro ya ardhi ni sawa kabisa na mgema tembo anayeangushwa na tawi (kuti) alilozoea kukalia kila siku huku akiamini kuwa ni imara kumbe limeoza.

Dk. Mwaiganju  anaeleza kwamba, serekali ya Tanzania pamoja na kwamba migogoro inaibuka siku hadi siku na kumalizwa kidiplomasia lakini bado suluhisho la kudumu halijatekelezwa ingawa lipo na linafahamika.

“Serikali bado haijachukua hatua madhubuti za utatuzi wa migogoro hiyo, kwani ili kuondoa migogoro ya wakulima na wafugaji lazima serikali ipime ardhi na kutenga maeneo ya wakulima, wafugaji na wawekezaji ikiwa ni pamoja na kumilikisha ardhi hiyo kwa vikundi vya wakulima na wafugaji”. Alisema Dk. Mwaiganju.

Unajua ngoja niwaeleze ndugu zangu, suala la elimu juu ya sheria za ardhi kwa hapa nchini ni sawa na ule usemi wa wahenga wetu kwamba, “Elimu kwaajili ya wajinga na Maisha ni kwaajili ya werevu”.

Anaendelea kueleza afisa huyo wa Ardhi mkoa wa Ruvuma kwamba, kwa mujibu wa sheria ya ardhi ya mwaka 1999 kifungu namba 5 kimetoa utaratibu  wa ugawaji wa ardhi kuanzia ngazi ya kijiji hadi Mkoa, lakini bado sheria na taratibu hizo zinavyunjwa.

Mfano, Taasisi ya Uwekezaji Tanzania imepewa nafasi ya kutoa ardhi isiyozidi ekari 500 kwa wawekezaji lakini cha kushangaza wawekezaji wamekuwa wakipewa zaidi ya hekari 5000 bila kujali maeneno ambayo yanategemewa na wakulima na ufugaji.

Hivyo ukilichunguza hilo kwa undani utaona kwamba elimu inayotolewa kwa wananchi ili watoe ardhi kwa waekezaji vijijini au katika hifadhi zilizotengwa kwaajili ya kilimo ni ile inayoongeza ujinga kwa wananchi na siyo inayolenga kumfanya awe mwerevu ili afaidi uhuru wake katika kuzitumia na kuzifaidi rasilimali zake.

Ndiyo maana anaeleza “Tanzania Elimu ni kwaajili ya Wajinga na Maisha ni kwaajili ya werevu” ambao wanapata ardhi bila kujali maisha ya mifugo ya wananchi katika eneo husika wala wakulima na matokeo yake migogoro inaibuka kila kukicha.

Anaeleza suluhisho katika matatizo ya migogoro ya ardhi ni jukumu la serikali kupima na kutenga ardhi kwaajili ya wakulima, wafugaji na wawekezaji.

Mfano hai afisa huyo anaeleza kwamba, angalia leo migogoro ya ardhi ikiwemo ile ya  wakulima na wafugaji , Wananchi wa kijiji cha Ligera wilaya ya Namtumbo  Mkoni Ruvuma, wapo katika mgogoro kati yao na wafugaji wavamizi waliotokea Mbeya na maeneo mengine ya  Morogoro.

Mgogoro huo, umesababisha pande hizo mbili kuishi katika hali ya wasiwasi bila kujua hatma ya maisha yao kwani wakati wowote machafuko yanaweza kutokea na hata kusababisha vifo.

Ama kweli “majani makavu hayakai karibu na moto”, hivyo ndivyo alivyaanza kueleza katibu tarafa wa tarafa ya Madaba halmashauri ya Songea aliyefahamika kwa jina la Dismas Komba. Alieleza kwamba, tatizo la migogoro ya  kimipaka kati ya wakulima na wafugaji linazidi kuwa kubwa siku hadi siku kwa sababu mkulima akilima mazao yake, mifugo ya wafugaji lazima ishambulie mazao hayo kwa kula.

Kwa mantiki hiyo lazima hapo ugomvi na mgogoro mzito utokee lakini endapo mifugo ingetengewa eneo la mbali la malisho na wafugaji hao basi hilo lisingeweza kutokea na ndiyo maana nimeanza na kusema ama kweli majani makavu hayakai karibu na moto na yakikaa lazima yaungue.

Hali hiyo inatokana na wananchi kujimilikisha ardhi kwa sababu serikali hajawajibika ipasavyo kayika kuhakikisha inapima na kutenga ardhi kwa ajili ya wakulima na wawekezaji.

Hivyo katibu Tarafa huyo anaeleza kwamba jambo la msingi analoliona yeye si vibaya kama serikali ingechukuwa maamuzi mazito kwanza ya kufuta hati milki zilizotolewa kwa wawekezaji ili waweke utaratibu upya wa kupima na kutenga ardhi kwa ajili ya makundi hayo matatu wakuli, wafugaji na wawekezaji.

“Ingekuwa uamuzi wangu ningefuta hati miliki zote za wawekezaji na za watu wakawaida ili serikali ipate nafasi ya kujipanga upya kuhusu ugawaji ardhi katika makundi hayo matatu”. Anaeleza afisa Tarafa.

Hata hivyo anaeleza kwamba, ni vyema serikali kwa kushirikiana na wadau wengine ikazingatia taratibu za uanzishaji vijiji, wilaya na mikoa kwa kuainisha bayana mipaka ya eneo husika itakayoambatana na kuyatenga maeneo kulingana na makundi hayo yanayoibua migogoro ya ardhi.
Kijiji cha Mkindo wilaya ya Mvomero mkoa wa Morogoro ni moja ya eneo la mfano wa migogoro ya ardhi iliyopata kutokea katika nchi hii kati ya wakulima na wafugaji kama anavyoeleza mmoja wa waathirika wa migogoro hiyo Edina Makubuli.

Migogoro hiyo imefikia hapo kwa sababu serikali inayo na inajua suluhisho la kudumu la namna ya kutokomeza tatizo hilo lakini kinachofanyika ni kufanya kazi kwa mazoea ameeleza makubuli.
Anaeleza msimamo huo wa serikali wa kufanya kazi kwa mazoea ndiyo unaosababisha migogoro kutokana na kukosekana kwa utawala bora ambao unapaswa kuangaliwa pia kwenye suala zima la umilikishaji ardhi kwa mwananchi na wawekezaji.

Viongozi hao hata kama watapewa taarifa mapema ya kutaka kutokea kwa mapigano kati ya wakulima na wafugaji, mara nyingi wanapuuzia na kusema hao waongo si jana tu tumetoka huko na wameelewana huo ni uzushi tu wa watu wachache.

Makubuli anaeleza matokeo yake jioni utasikia makundi hayo yamechapana, wengine kuuawa na kujeruhiwa. Hapo ndipo utakapoona viongozi wanajitokeza kwa ajili ya kuhalalisha posho na si kulipatia suluhisho la kudumu tatizo.

Anaeleza tatizo hapa linasababishwa na viongozi wa serikali ambao wanapata taarifa mapema lakini wanachelewa kufika eneo la tukio kwa wakati na matoke yake yanakuwa mabaya.

Pia hata wanapofika hakuna hatua madhubuti zinazochukuliwa zaidi ya kulifanya jambo hilo kana kwamba mgonjwa anayeumwa malaria akapewa dawa aina ya Panaldo ya kutuliza maumivu na si kupewa dawa ya kutibu ugonjwa husika.

“Kwa kufanya hivyo mimi kama mmoja kati ya walioathiriwa na migogoro hiyo ninaona kabisa jambo hili serikali inalifanya kama mradi wao wa kujipatia pesa za safari kwaajili ya kuelekea kwenye tatizo kwa lengo la kutuliza na si kutibu tatizo”. Alieleza Makubuli.

Anachoamini yeye ni kwamba serikali inatumia migogoro ya wakulima na wafugaji kama miradi bubu ya kuhujumu uchumi wa nchi na kama si hivyo kwanini wasipime na kutenga maeneo ya makundi hayo? Alihoji Makubuli.

Pia alihoji hivi ni kiasi gani cha fedha kinatumika kufuatilia migogoro hiyo na kwa miaka  mingapi sasa ambapo bado suala hilo halijapatiwa ufumbuzi wa kudumu? Ama kweli Elimu kwaajili ya mjinga na maisha ni kwaajili ya werevu.


ARDHI ni rasilmali muhimu sana katika maendeleo ya binadamu, Mwalimu Nyerere  enzi za uhai wake alisema. “ili kupata maendeleo tunahitaji mambo makuu manne, ardhi, siasa safi, watu,na uongozi bora”. Kauli hii ilikuwa na lengo la  kuonyesha umuhimu wa ardhi katika suala la maendeleo endapo itatumika na kusimamiwa ipasavyo.

No comments:

Post a Comment